JE, UNAFAHAMU KUWA SERIKALI YA TANZANIA IMEONGEZA NAFASI ZA AJIRA KWA WATUMISHI WA SEKTA YA AFYA NA USTAWI WA JAMII?
- Katika kuboresha utoaji huduma bora za afya nchini na Ustawi wa Jamii, Serikali ya Tanzania imeendelea kutoa kipaumbele kwa kuongeza idadi za ajira, kwa watumishi wa afya na ustawi wa jamii nchini, ikitumia mikakati mbalimbali.
- Ili kuziba pengo la asilimia 62% la uhaba wa watumishi wa afya na ustawi wa jamii, Serikali ilipanga kuongeza idadi ya watumishi kulingana na bajeti iliyotengwa kila mwaka, pamoja na maombi ya vibali vya ajira yanayowasilishwa na Halmashauri mbalimbali nchini.
- Kuanzia Julai 2005 hadi Juni 2010, jumla ya vibali vitano (5) vya ajira ya watumishi wa afya na ustawi wa jamii wa kada na ngazi mbalimbali vimetolewa na Serikali, vyenye idadi ya watumishi 23,502 kwa ngazi ya Taifa, Kanda, Mikoa na Halmashauri.Katika vibali hivyo, takriban asilimia 70 ya nafasi zilizotengwa, zilijazwa na watumishi ambao walipangiwa kazi kwenye vituo vya kazi mbalimbali nchini (Takwimu kutoka WAUJ, 2010).

MAENEO YANAYOHITAJI UIMARISHAJI
Pamoja na jitihada hizi za Serikali na wadau wengine, yapo maeneo muhimu yanayohitaji kuimarishwa:
- Serikali na wadau wa Sekta ya Afya na Ustawi wa Jamii waongeze vyuo zaidi na uwezo wa vyuo kudahili na kutoa wahitimu wengi zaidi, wenye taaluma mbalimbali za afya pamoja na kubuni na kuimarisha mifumo ya kuwapangia kazi baada ya kuhitimu masomo, kuwafikisha kwenye vituo vyao vya kazi na kuwafanya wabakie huko.
- Halmashauri zitoe taarifa mapema, kwa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, kuhusu idadi na aina ya kada ya watumishi wapya, walioripoti kwenye vituo vya kazi.
- Halmashauri ziweke takwimu sahihi ili kupata mwelekeo wa watumishi wanaoripoti na kubaki katika vituo vyao
- Kuendelea kuelimisha Halmashauri zote juu ya umuhimu wa kuwa wabunifu wa kutengeneza mikakati ya kuvutia na kubakiza watumishi wa afya na ustawi wa jamii kwenye vituo. Vivutio hivyo pia viwekwe wazi kwa jamii.
- Halmashauri kuhamasisha wadau wote wa sekta, kuchangia katika ajira ya watumishi kwa Mikataba kwa muda na hatimaye kuwaingiza katika ajira ya Serikali kama mpango wa muda mrefu, wa kuongeza idadi ya watumishi.
Ujumbe huu umetolewa na Taasisi ya Mkapa Foundation, kupitia Tanzania Human Resource Project, kwa msaada wa Watu wa Marekani,kupitia Shirika la Misaada la Marekani (USAID)


